• KIBAYACLASSIC

    The voice of Africa

    Wednesday, May 17, 2023

    NYANSAHO AWASHIKA MKONO CWT SERENGETI..

     

    NYANSAHO AWASHIKA MKONO CWT SERENGETI, WALIMU 1753 KUFAIDIKA JIKO LA GESI MASHULENI

    Chama cha walimu (CWT) wilayani Serengeti kupitia kitengo cha wanawake kimefanikiwa kuwezesha upatikanaji wa majiko 190 kutoka kwa mdau wa maendeleo Ndg.Rhimo Nyansaho kupitia Taifa Gesi,upatikanaji wa gesi hizo zitasaidia katika uhifadhi wa mazingira na kuokoa muda wa walimu katika kujipatia chakula wawapo shuleni na kufaidisha walimu 1753.

    Akikabidhi majiko hayo ya gesi kwa walimu wawakilishi mahala pa kazi kutoka shule 190 mkuu wa wilaya ya Serengeti Dkt.Vincent mashinji amempongeza Ndg.Nyansaho kwa kushirikiana na Taifa gesi kwa kutoa majiko hayo ya gesi 

     ‘’ Tumepata majiko 190 tunawashukuru sana Taifa gesi,naomba mtuletee na gesi zingine ikiwezekana na kwenye magereza mkatusaidie tuweze kuweka gesi tupunguze uharibifu wa mazingira naomba wanaserengeti tukubaliane kimsingi pale tunapopata vijana wanaotoka kwenye maeneo yetu,ambao wanapenda kutuletea maendeleo tuache maneno ya kuwakatisha tamaa,’’, amesema mashinji

    Aidha ,Dkt.Mashinji amewapongeza wadau mbalimbali wa maendeleo kwa kutoa misaada yao katika nyanja mbalimbali za kimaendeleo wilayani Serengeti na kutoa wito kwa wakazi wa Serengeti kuwapa ushirikiano wadau wa maendeleo.

    Naye Mwenyekiti wa CWT wilaya ya Serengeti Mwl.Lusawi Mayala amekipongeza kitengo cha walimu wanawake kwa kuvulia njuga upatikanaji wa majiko hayo ya gesi,aidha amewakumbusha walimu waliofaidika na msaada huo wa majiko kuwa majiko hayo pia ni zana za kufundishia hususani katika kuelemisha wanafunzi juu ya nishati safi na faida za matumizi ya nishati hiyo ili kuondoka na uharibifu wa mazingira.

    Kwa upande wa Mwenyekiti wa CWT kitengo cha wanawake Mwl.Rahabu Mgesi amesema’’katika ziara tulibaini kwamba walimu wengi wanakaa nje na vituo vya kazi,ili kuleta ufanisi katika majukumu yao tukaona ipo haja ya kutafuta majiko ya gesi ili kuweza kuharakisha walimu kupata chai wawapo shuleni’’

    Katibu CWT Mkoa wa Mara Susane Shesha amemshukuru Ndg.Nyansahao kwa namna alivyojitoa katika kutoa msaada wa majiko hayo ya gesi,na amewataka walimu kutunza majiko hayo ili yaweze kudumu.


    Awali akisoma risala kwa mgeni Rasmi katibu wa CWT kitengo cha wanawake Mwl.Grace Mutaengerwa amesema ‘’kitengo cha walimu wanawake kwa kutambua michango ya walimu katika kuinua kiwango cha elimu na uhifadhi mazingira kiliwasilisha maombi yao ya msaada ya kupatiwa majiko ya gesi kwa mdau wa elimu Rhimo Nyansahao,Mdau huyu kwa kushirikiana na Taifa gesi wamewezesha shule zote 190 kupata majiko ya gesi’’


    Hafla hiyo fupi ilijumuisha viongozi mbalimbali wa Serikali,Chama cha walimu Mkoa wa Mara na Serengeti, pamoja na taasisi mbalimbali zilizopo wilayani Serengeti.

    No comments:

    Post a Comment